Saturday, September 11, 2010

Uzuri Wa Mkakasi...

Mbona kilio mwanangu nakuuliza nambie? Ukilia unavyofanya nani atanipanguza mimi yanayonitiririka rohoni mwangu? Maisha yana majaribu yake lakini mbona kukinai matumaini? Mambo huenda yakaenda sege mnege moja baada ya mengine utadhani umerogwa. Marafiki huenda wakahepa ukabaki hauna yeyote kukuondolea upweke. Marafiki hawa hawakuwepo ulipozaliwa kwa hivyo mbona uukubalishe moyo wako kuweweseka na dhana hiyo? Usidhoofike mwanangu, sitakwacha mie niliyekuleta humu duniani, Sharti. Nitasimama nawe hadi nisiweze kufanya hivyo tena, mwanangu. yavute machozi yako mwanangu. Tafadhali nisikize unirejeshee raha moyoni mwangu mwanangu. Sijapata kuondoka ninapoketi kwa siku mbili nikikutizama wewe mwanangu. Ongea uniambie lolote angalau mwanangu. Usilie tena mwanangu ukilia utaniletea maradhi pia. Maradhi ya moyo. Mungu nimemwomba, nikamwomba na nikamwomba tena lakini yaonekana inabidi nisali tena na tena. Tafadhali koma kilio mwanangu, Mumbu husaidia anayetamania kusaidiwa. Nitaimba wimbo huu hadi sauti inipotee Sharti mwanangu.

Tuesday, July 13, 2010

Dibaji

Ninaandika visa hivi nikiwa na lengo moja hususan. Kuandika kwa minajili ya kuwavutia watu wowote wale wanaoienzi lugha hii mufti ya Kiswahili. Kiswahili nakienzi kwa mvuto usioweza kumithilishwa na lugha yeyote ile. Kiswahili utamu wake umezidi utamu wowote ule ambao umewahi pitia kwenye ulimi wangu.

Kiswahili kitukuzwe.